Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Fedha Agnes Kuhenga.
23/1/2018 Balozi za Israel na
Ujerumani hapa nchini zimeahidi kuendelea kushirikiana na Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) ili kuhakikisha watanzania hasa watoto wanapata huduma
bora za matibabu ya moyo.
Hayo yamesemwa leo na Manaibu
Balozi wa nchi hizo walipotembelea Taasisi hiyo leo ili kuona maendeleo ya kambi
maalum ya matibabu ya moyo kwa watoto inayofanywa kwa pamoja na madaktari
bingwa wa Moyo kwa watoto wa JKCI, Israel na Ujerumani.
Matibabu hayo ya magonjwa ya
moyo ya kuzaliwa nayo yanatolewa kwa watoto wenye umri wa kuanzia mwezi mmoja
hadi miaka 18 yanafanywa kwa njia ya upasuaji wa bila kufungua kifua
(Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab.
Naibu Balozi wa Ujerumani nchini
Mhe. Jörg Herrera alisema kuwa nchi yake
imekuwa ikishirikiana na Tanzania katika mambo mbalimbali ya maendeleo ikiwemo
afya hivyo basi watafanya kila wanachoweza ili kuunga mkono jitihada za kuimarisha afya hapa
nchini.
“Nimetembelea leo Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete ili kuona kambi ya pamoja ya upasuaji wa moyo inayofanywa na
madaktari wa JKCI, Israel na Ujerumani
nimefurahi kuona kazi nzuri ya kiwango
cha kimataifa inayofanyika hapa ya kuokoa afya za watoto”.
“Wanafanya upasuaji wa bila
kufungua kifua kwa watoto wenye matatizo ya moyo nafikiria kuimarisha zaidi mahusiano tuliyokuwa nayo ili tuweze kuokoa maisha ya watoto wengi zaidi
kwa faida ya kizazi kijacho”, alisema Mhe. Naibu Balozi Herrera.
Naye Naibu Balozi wa Israel nchini
Mhe. Michael Baror alisema nchi yake inajivunia
kuwa sehemu ya watoa huduma wa matibabu hayo wataendelea kubadilishana
uzoefu wa kazi kwa kuwaleta madaktari ambao watafanya kazi na wataalamu waliopo
hapa nchini hii ikiwa ni moja ya kuimarisha mahusiano baina ya nchi hizi mbili.
“Tumekuwa tukifadhili elimu za madaktari na wauguzi wanaotoka JKCI
na kuja kusoma nchi kwetu vilevile tunatoa matibabu kwa watoto wenye matatizo
ya moyo ambao wengine tunawatibu hapa nchini na wengine wanatibiwa nchini
kwetu. Nafurahi kuona mahusiano yetu yanafanikiwa na kuimarika zaidi naamini
wataalamu hawa wa afya wanapata ujuzi wa kutosha zaidi”, alisema Naibu Balozi
Mhe. Baror.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi
wa Idara ya Magonjwa ya Moyo ambaye pia
ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo Peter Kisenge alisema kambi hiyo ya siku
sita inafanya upasuaji wa bila kufungua kifua kwa kuziba matundu ya moyo kwa watoto wenye umri
wa mwezi mmoja hadi miaka 18.
Dkt. Kisenge alisema kuwa
madaktari hao kutoka Ujerumani na Israel wanafanya upasuaji wa kuziba matundu
na kutoa mafunzo kwa madaktari wa JKCI ya
jinsi ya kuziba matundu ya moyo kwa watoto na kuwahudumia watoto wenye
matatizo hayo.
Tangu kuanza kwa kambi hiyo tarehe
20/1/2018 jumla ya watoto 32 wamefanyiwa uchunguzi na watoto 10 wamefanyiwa
upasuaji wa kuziba matundu ambapo hali
zao zinaendelea vizuri na wataruhusiwa
pindi afya zao zitakapoimarika.
Post a Comment